Watu watatu wamekufa papo hapo wawili
wa familia moja na wengine watatu kujeruhiwa vibaya baada ya kupigwa na
radi wakati wakifanya ibada chini ya mti katika kitongoji cha Mtakuja,
kijiji cha Kivingo, kata ya Longuza, wilayani hapa.
Tukio hilo lilitokea juzi saa 10:30 jioni huku kukiwa na upepo mkali uliombatana na manyunyu ya mvua.
Afisa Tarafa ya Umba, Mpemba Gabriel, aliwataja waliokufa kwa kupigwa na
radi hiyo kuwa ni Esther Moleto, Salome Sengasu na ndugu yake Naiyo
Sengasu.
Gabriel alisema kuwa majeruhi wamelazwa katika Kituo cha Afya cha Mnazi kwa matibabu.
“Walikuwa chini ya mti wakiendelea na ibada ghafla hali ya hewa
ilibadilika na kuibuka upepo mkali ulioambatana na mvua,” alisema
Gabriel.
Naye Afisa Tarafa ya Mlalo, Dunstan Mudu, alisema kuwa kabla ya tukio
hilo kulikuwa na ngurumo za radi zilizoambatana na upepo mkali.
Mudu alisema hali hiyo iliwatisha wakazi wa maeneo hayo na kulazimika
kuacha shughuli zao kisha wakajifungia ndani ya nyumba zao.
Kufuatia tukio hilo, viongozi wa serikali wa ngazi za kata, tarafa hadi
wilaya ya Lushoto, wamewashauri wananchi kutokaa karibu na miti wakati
mvua zinaponyesha.
Alisema wilaya ya Lushoto imezungukwa na milima na misitu ya asili ambayo ni kichocheo kikubwa cha radi.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Kata ya Longuza, Sadick Singano, alisema
wilaya ya Lushoto imezungukwa na milima mingi huku makazi ya watu
yakiwa chini.
Sungano alisema kuwa kwa kawaida radi hufuata miti na kuwataka wanaolima mabondeni kuwa makini kwani lolote linaweza kutokea.
No comments:
Post a Comment