HABARI MOTO MOTO ...

Monday, November 12, 2012

Askari wastaafu JWTZ watapeliwa Z`bar

Askari wastaafu 700 wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), visiwani Zanzibar wametapeliwa na kuamua kupitisha azimio la kumshitaki aliyekuwa Mwenyekiti wa Muungano wao, (Muwawata), Sajuni Taji Mstaafu Asseyd Mayungi.
Wapinganaji hao wastaafu wametapeliwa mamilioni ya fedha zikiwemo ada za uanachama za kujiunga na muungano wao pamoja na fedha za gharama za kuanzisha vikundi vya wajasiriamali katika kupambana na ukali wa maisha baada ya kumaliza utumishi wa umma.
Hayo yamefahamika katika mkutano wa wanachama wa Muungano huo kutoka Mikoa mitano ya Zanzibar uliyofanyika Amani, Mkoa wa mjini Magharibi Kisiwani Unguja na kuhudhuriwa na Mwenyekiti wa muda wa Muwawata, Brigedia Jenerali Mstaafu Haroun Othmani.
Akisoma azimio la mkutano huo, Mwenyekiti wa Muwawata, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Sajenti Mstaafu wa JWTZ Miraji Kiongwe, alisema wanaunga mkono kuondolewa madarakani kwa Sajuni Taji mstaafu Mayugi kutokana na tuhuma za ubadhirifu wa fedha za muungano huo.
“Mikoa mitano ya Zanzibar kama wanachama tunaunga aliyekuwa Mwenyekiti wetu Asseyd Mayungi kuondolewa uongozi kwa tuhuma za kuhusika na ubadhirifu wa fedha za Muwawata,” alisema Kiongwe.
Alisema baada ya wanachama kujadili kwa kina ripoti ya ubadhirifu wa fedha za Muwawata wamekubaliana kila kikundi cha ushirika kilichotapeliwa fedha kufungua kesi haraka dhidi ya Mayungi na watu alioshirikiana nao kufanikisha mpango huo.
Kiongwe alisema Mayungi anatuhumiwa kuzunguka katika mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Zanzibar na kukusanya mamilioni ya fedha kama ada za kujiunga na Muwawata pamoja na fedha za kusajili vikundi vya Ushirika vya askari wastaafu kabla ya kupatiwa mikopo.
Alisema kwamba kazi hiyo alikuwa akiifanya kwa kushirikiana na Taasisi moja ya kusadia Wajasiriamali (jina lake linahifadhiwa) ambao walifika Zanzibar na kufanikiwa kukusanya fedha kutoka vikundi 18 vya ushirika.
Alisema Mayungi kwa kushirikiana na Taasisi hiyo jumla ya Sh. 23,880,000 zimekusanywa na kutumika tofauti na malengo ya Muwawata.
Kiongwe alisema kwamba tangu kukusanywa fedha hizo mwaka jana wamekuwa wakifuatilia maendeleo ya mikopo bila ya mafanikio kwa Taasisi hiyo ya kusaidia wajasiriamali na kubainika kuwa tayari wametapeliwa.
Akizungumza katika mkutano huo Mwenyekiti wa Kamati ya mpito ya Uongozi wa Muwawata, Brigedia Jenerali Mstaafu Othman, aliwataka wanachama wa Muungano huo kuwa na moyo wa subira wakati tatizo hilo likishughulikiwa na uongozi wa mpito kabla ya wahusika kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Hata hivyo aliwataka kuendelea kuunga mkono viongozi walichaguliwa kwa muda kuongozi ili kuhakikisha malengo ya kuanzishwa kwa Muungano huo yanafanikiwa na kuwanufaisha wanachama wake.
Juhudi za kuwapata Asseyd na Taasisi ya kusaidia wajasiriamali ambazo zimekubwa na kashfa ya kuwatapeli wastaafu hao wa JWTZ hazikuweza kuifanikiwa kupitia simu zao za na barua pepe.

No comments:

Post a Comment