
Kundi la kwanza la wachezaji na viongozi wa timu ya AS FAR ya Morocco
inayokuja kuivaa Azam katika mechi yao ya kwanza ya raundi ya pili ya
michuano ya Kombe la Shirikisho kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es
Salaam Jumamosi liliwasili nchini jana mchana.
Akizungumza na NIPASHE, Afisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania
(TFF), Boniface Wambura, alisema kuwa kundi hilo liliwasili saa 8:00
mchana kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar
es Salaam na kuongeza kuwa kundi la mwisho la kikosi hicho litatua
nchini leo mchana.
Wambura aliongeza kuwa maandalizi ya mechi hiyo yako katika hatua za
mwisho na wanaamini kuwa Azam watafanya vyema katika mechi hiyo na
kujiwekea mazingira mazuri ya kusonga mbele kwenye mashindano hayo
wakiwa ni wawakilishi pekee wa Tanzania waliobaki katika michuano ya
kimataifa.
Alisema vilevile kuwa marefa wa mechi hiyo walioteuliwa kutoka
Shelisheli ambao ni Emile Fred atakayepuliza filimbi akisaidiwa na Steve
Maire na Jean Ernesta na wa mezani, Jean Claude Labrossa watatua nchini
keshokutwa.
Alimtaja Kamishna wa mechi hiyo kuwa ni Abbas Sendyowa kutoka Uganda ambaye pia atatua nchini keshokutwa.
Azam inayoshiriki michuano hiyo ya Shirikisho la Soka la Afrika (CAF)
kwa mara ya kwanza, imefika hatua hiyo baada ya kuzitoa Al Nasri ya
Sudan na Barrack Young Controllers ya Liberia.
Simba iliyokuwa ikiiwakilisha Tanzania katika Ligi ya Klabu Bingwa
Afrika ilitolewa hatua ya awali na Recreativo de Libolo ya Angola kwa
kipigo cha jumla cha mabao 5-0.