HABARI MOTO MOTO ...

Sunday, January 26, 2014

Mfuko wa Rais wakumbwa na kashfa

Mfuko  wa Rais wa Kujitegemea (PTF) umekumbwa na kashfa nyingine baada ya kudaiwa kuwadhulumu wanachama wake akiba zenye thamani ya zaidi ya milioni 10/-.
Wanachama hao ambao ni kikundi cha Mbezi A na B wamedai kuwa mpaka sasa imeshapita miaka mitatu wamekuwa wakipigwa kalenda kila wakati kuwa watapatiwa akiba zao jambo ambalo limeshindikana kutekelezeka.

Malalamiko hayo ambayo yametolewa na Mwenyekiti wa kikundi cha Mbezi A, Mahija Yusuph, alisema kuwa wanashindwa kuelewa ni kwa nini mfuko huo unawacheleweshea kuwapa akiba zao wakati tayari wameshamaliza kulipa mkopo.
Alisema kuwa tangu mwaka 2010 walitakiwa kupatiwa akiba zao na matokeo yake kila wakati wanaambiwa wasubirie bajeti ipitishwe na ikishapita, hawapatiwi fedha zao.
Yusuph alisema kuwa kuna wengine walijaza fomu za kupatiwa mkopo lakini mpaka sasa hawajapatiwa. “Sisi tuliwauliza akiba zetu mmekaa nazo kwa muda mrefu vipi mtatulipa na riba lakini wametukatalia na kusema kuna baadhi hawakumaliza mkopo tukawajulisha watukate hilo deni la wenzetu na kiasi kilichobakia watulipe fedha zetu lakini tunapigwa kalenda,” alisema.
Alisema kuwa kabla ya kulazwa hospitali kwa mwezi alifuatilia fedha hizo na kujulishwa zitatolewa Januari mwaka huu kuanzia tarehe 2 jambo ambalo halikufanyika.
Alisema aliporuhusiwa kutoka hospitali alifuatili fedha hizo na kujulishwa kuwa wasubirie wiki mbili.
Yusuph alisema idadi ya watu waliokuwapo kwenye kikundi hicho walikuwa 40 na kwa sasa wamepungua nakufikia 20 kwa kuwa wameona hawana imani na mfuko huo.
Naye Katibu wa kikundi hicho, Rehema Marima, alisema kuwa mfuko huo huenda ukawa umekufa lakini hawapo wazi.
Alisema baada ya kumaliza mikopo yao wengine walijaza fomu za mkopo lakini mpaka sasa miaka mitatu imepita hawajajulishwa jambo lolote.
Marima alisema wao wanachokitaka ni kupatiwa akiba zao kwani wamechoka kupigwa kalenda kila wakati na kupoteza muda wao kufuatilia.
Alisema kuwa siyo kikundi chao tu kinachodai wapo wanachama wengi wanaodai na hawajui hatima yao ni nini.
Hata hivyo, alisema na kikundi cha Mbezi B kinawadai akiba zao na wenyewe hawajui nini hatima ya fedha zao.
NIPASHE ilizungumza na Mkurugenzi wa PTF, Haigath Kitala, ambaye alieleza kuwa mfuko wake unatambua akiba zinazodaiwa na wanachama wake na kwamba watakapopata watazitoa kwa wakati.
Alisema kuwa mfuko upo hai na wanatambua madeni ya wanachama wake kwani wana kumbukumbu ya kila mwanachama.
Kitala alisema taarifa aliyonayo ni kwamba kituo cha Mbezi A, wanadai akiba zao za Sh. milioni 8.17 na wenyewe wanadaiwa mkopo wa Sh. milioni 4.25 ambazo wanachama wake hawakuzirejesha kama wanavyotakiwa. 
Alisema kwa upande wa kituo cha Mbezi B, wanadai akiba ya Sh. 8,963,400 na mfuko huo unawadai Sh. 7,526,400.
Kitala alisema kwa wale ambao wanadai akiba zao wanatakiwa kufika ofisini kwao kwa ajili ya kupatiwa taarifa na siyo kusikiliza wasiohusika.
Alisema kwa sasa mfuko unasubiri kupatiwa fedha ili waanze kulipa madeni hayo kwani kuna matawi mengine ambayo yanadai fedha.
Madhumuni ya Mfuko wa PTF ni kuwasaidia wananchi wa kipato cha chini kwa kutoa mikopo yenye riba nafuu ili waweze kujikwamua kimaendeleo.

No comments:

Post a Comment